user_mobilelogo

Party Emblem

Party Flag

 

Youth League

Contact us


Communist Party Marxist - Kenya (CPM-K)
This email address is being protected from spambots. You need JavaScript enabled to view it.
P.O Box 101011-00101 Nairobi, Kenya.
 

Let's Get Social

          

 

Related Social Links

 Revolutionary Youth League (RYL)
   
 Revolutionary Student Commission
    
 Revolutionary Women League
 Pio Gama Pinto Institute 

Support CPM-K 

membership

Publications

 

 

 Grab a Copy

 

CPM-K Memberships

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Siku Kuu ya Mashujaa wa Uhuru

 

Ilikuwa tarehe 20 Oktoba na mwaka ni wa 1952

Wakoloni walipoamua kuzidisha njama zao

Za kuwavamia wazalendo wana halisi wa taifa letu

Waliyokuwa wameamua kujitolea kuutetea utu wa mtu mweusi

Wakizunguka kote nchini kutangaza mapambano ya uhuru

Huku wakifichua wasaliti vibaraka wa wakoloni

Na kiapo wakilishana kiapo chenyewe cha kuapa

Kenya ni nchi ya Wakenya Wazungu warudi kwao

Tunapigania uhuru na ukombozi tunadai mashamba yetu

Ni haki yetu kujitawala tunataka kujiamulia sudi yetu wenyewe

Ila haki hatutapewa kama zawadi na wakoloni

Itatupasa kuipigania kwani uhuru utadai hata damu yetu

Kwa hivyo tujizatiti tuwe tayari kwa vita vigumu na vikali

Wala hatutorudi nyuma tutapigana mpaka tutakapojikomboa

Wakoloni wakasikia kuhusu kiapo cha kuwaunganisha wadhulumiwa

Wakaogopa sana wakatetemeka kwa hofu na dukuduku

Sauti madhubuti ya wananchi ikautingisha ukolonimkongwe

Serikali ya kikoloni na walowezi na machifu na mahomugadi wote

Wakashindwa kutawala kunyonya na kusaliti kwa amani

Wakawa wanasaka wanakamata wanafunga wanaweka vizuizini wazalendo

Viongozi wa mapambano ya uhuru wasiweze kulala majumbani mwao

Kifagio cha polisi na askari kanga kikakusanya wananchi kwa maelfu

Hali ya hatari ikatangazwa maanake vita moto dhidi ya Wakenya wote

Nyakati za ufashisti wa Wingereza dhidi ya taifa letu

Zikatangazwa rasmi na dola la ukoloni nchini kwetu

Njia zote za kudai uhuru kwa amani zikafungwa kabisa zikazibwa rasmi

Ndipo kibirikizi kikalia wazalendo wakakusanyika

Wafanyikazi na wakulima wa Kenya wakasema wakati umewadia

Sisi pia ni binadamu wenye akili na damu kama wao

Kwa vile tunakufa hatutoendelea kukubali kufa kikondoo

Maana wameamua kutuchinja tunakataa kuzidi kuchinjwa kama nguruwe

Tunasema potelea mbali dawa ya moto ni moto

Mwenye bunduki aanze kupiga na wa bomubomu alipue

Wa panga atoke na panga na wa mkuki na mkuki wake

Masogora wa vita wakati wa kuonyesha ufundi wenu umefika

Kuanzia hivi leo ni kufa ama kupona hadi ukombozi wa taifa letu

Maadui ni wakoloni walowezi na machifu na mahomugadi wao

Jeshi la Uhuru na Mashamba likatangaza vita vya kigorila

Umashuhuri wa Mau Mau ukaanza kuenea nchini na duniani kote

Basi tukumbuke siku hii si ya mahomugadi wa jana na leo

Si siku ya waoga na wasaliti walotumiwa na adui dhidi yetu

Si siku ya serikali inayoukumbatia na kuubusu ukolonimamboleo

Si siku ya wanyonyaji na wabakuzi wa mashamba na maploti

Wala si sahihi kuiita Kenyatta Dei aliyekufa akiwa msaliti mkuu

Ni siku kuu ya kitaifa ya kuwakumbuka mashujaa wa uhuru

Ni siku ya Jeshi la Uhuru na Mashamba siku kuu hii ni ya Mau Mau

Ni siku ya kutukumbusha uhuru wa kitaifa hudai kujitolea mhanga

Na kwamba ukombozi bado kwani ukolonimamboleo ungaliko

Ushahidi wake ni kwamba hivi leo tuko gerezani

Siku kuu hii

Kwa mara nyingine tena

Ninalazimika kuisherehekea jela

Mimi na wazalendo wengine

Siku Kuu ya Mashujaa wa Uhuru

Tunaikumbuka tukiwa wafungwa wa kisiasa

Tuko gerezani wakati huu

Kwani tunaitikia mwito wa mashujaa wa uhuru:

Pambana siku zote pambana!

Pambana hadi ukombozi kamili wa kijamii na kitaifa!

 

Mwandawiro Mghanga

Jela Kuu ya Kibos   Oktoba 20 1988

 

 

Tuwakumbuke Mashujaa Wetu

 

Tuwakumbuke

Mashujaa wa nchi yetu

Wazalendo halisi wa Kenya

Jinsi walivyokuwa wamejitolea mhanga

Kupambania uhuru na ukombozi wa nchi yetu:

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu ya kila aina

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Tuwakumbuke mashujaa wa Pwani ya nchi yetu

Wazalendo wa Mombasa na Malindi na Lamu

Na Siu na Pate na Vanga

Ambao mamia ya miaka iliyopita

Walikufa wakipambana

Wakipambana dhidi ya uvamizi wa Waarabu

Waliyokataa kutawalwa na wageni

Waliyoupiga vita uvamizi wa kikatili wa Wareno

Wareno wakashindwa kabisa kupenya hadi bara

Tukumbuke kuwa ngome

Inayoitwa Fort Jesus

Ambayo sasa ni jumba la ukumbusho Mombasa

Ngome ni taswaira ya uvamizi wa Wareno nchini

Ni ushahidi wa upinzani kutoka kwa mababu na mabibi zetu

Ni ukumbusho wa nyanyaso na gandamizo

Za Wazungu wa kwanza kujaribu kutawala Kenya

Ngomeni maelfu ya Wamijikenda na Waswahili walifungwa

Ngomeni wazalendo wa nchi yetu waliteswa

Ngomeni damu ya mashujaa ilimwagika

Tumtaje Shee Mvita, mfalme wa mwisho wa Mombasa

Aliyeuawa na Wareno

Akiutetea uhuru na ukombozi wa watu wake

Mfano wa bei ghali iliyolipwa na wazalendo

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Mwangeka

Wawa Mwangeka wa Mwanda Njawuli

Mzalendo kutoka Vuria

Kilele cha milima ya Dawida

Milima ya juu zaidi Mashariki mwa Kenya

Inayosifika kwa uzuri wake usiyo na kifani

Kule kulikopandishwa bendera ya uhuru wa Kenya Pwani

Ing'oni Mwangeka mzaliwa sehemu hii ya nchi yetu

Naye anatajika, ni mtu mashuhuri

Kwa uzalendo na ushujaa

Kwa kuongoza maaskari hodari wa Dawida

Waliyowaeleza wakoloni kwa mikuki, nyuta na mishale

Nyinyi ni nani mnaotamba katika nchi yetu?

Hii ni ardhi yetu kutoka kale na zamani

Tutaitetea hata kwa damu kumwagika

Tunapinga kutawalwa na wageni

Tuko kwa nchi yetu tunawezaje kuwafanyia kazi?

Tunaishi kwa jasho letu wenyewe

Basi itakuwaje tuwe wapagazi wenu?

Tu watu kama nyinyi tutakubalije kuwa watumwa wenu?

Tuna lugha, dini, mila na tamaduni zetu hatuna haja na zenu!

Kina Mwangeka wakatangaza vita dhidi ya vita vya wakoloni

Wakapigana wakapigana wakapigana bila kurudi nyuma

Mwangeka na maing'oni wa Dawida

Wakakataa kufa wakipiga magoti

Wakadinda kuwainulia maadui mikono yao

Wakafa wakiwa na silaha mikononi

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Halafu kuna Me Kitilili

Me Kitilili Me Kitilili Me Kitiliii

Me Kitilili wa Menza

Me Kitlili mwanamke shujaa kutoka Ugiriamani

Mzalendo Me Kitilili na Wanje, Wanje wa Mwadorikola

Jazanda ya uzalendo wa wanawake wa nchi yetu

Waliyowaongoza wanaume na wanawake wa Ugiriamani

Kuuasi na kuulani ukoloni kwa maneno na vitendo

Kukataa kuwa maaskari wa wakoloni

Kugoma kufanywa mahamali wa mabeberu

Kudinda kunyang'anywa ardhi yao

Wakoloni wakawashambulia kikatili kikoloni

Wanje wa Mwadorikola na Mee Kitilili

Wakawaongoza wanaume kwa wanawake

Kutetea mila na tamaduni za Wagiriama

Kulinda hadhi ya mtu mweusi, heshima ya Mwafrika

Wakoloni wakawaita wanawake mashujaa wetu wachawi

Wakakashifiwa wakakamatwa wakadunishwa wakateswa

Mama zetu wakahamishwa hadi nchi ya Wakisii

Bali Me Kitilili na Wanje wa Mwadorikola

Wakasimama madhubuti wasitingishike wasikate tamaa

Wakatoroka na kujasiri mamia ya kilometa

Wasiogope hatari za nyika na misitu na wanyama tilatila

Wakarudi Ugiriamani kuendelea na mapambano

Wakaendelea kuongoza harakati dhidi ya ukoloni

Wakatukanwa wakapakwa matope wakazuiwa wakafungwa

Wakahamishwa hadi Kisimayu

Bali mama zetu milima ya ushujaa na uzalendo

Mfano wa ukakamavu na kujitolea mhanga

Wakakataa kusalimu amri za wakoloni

Wakatetea uhuru wa nchi yetu na watoto wao daima

Wakaishi wakiwa mihimili ya umoja wa watu wao

Wakawa sehemu ya nguzo ya historia ya ukombozi wa Kenya

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Huko Unandini Koitaleli ni mashuhuri

Koitaleli, kiboko cha kiburi cha wakoloni

Wanandi kwa mikuki na ngao mikononi

Wakawauliza wakoloni:

Hii ni nchi yetu kutoka tangu na tangu

Nani amewaruhusu kujenga reli hapa?

Mnawezaje kuingia na kupita kwetu

Bila hata hodi wala hamjambo!?

Mna njama gani juu ya ardhi yetu

Ambapo tumekuwa tukiishi tangu kale na zamani!?

Wakoloni kwa kiburi kujitapa na kujisahau

Wakajibu kwa bunduki na bomubomu

Kwa kuua na kuchinja pasina kutangaza vita

Wanandi wakatahamaki wakajizatiti sawasawa

Wakasema hawa watu ni wa sampuli gani?

Watu gani hawa wasiyo na utu heshima wala adabu!

Ni binadamu gani hawa wasiyojali maisha?

Hawajui lugha nyingine ila vita na madharau tu?

Basi, imetupasa kupigana nao

Kwani nasi hatuna utamaduni wa woga

Ndipo Wanandi wakajiandaa ipasavyo

Kwa mikuki na ngao wakajumuika

Mabingwa wa vita vya kigorila wakajipanga barabara

Wakawa wanawavizia na kuwashambulia ghaflaghafla wachokozi

Kina Koitaleli wakawachapa wavamizi hadi wakasarenda

Wakatapika kiburi chao wakaomba majadiliano

Mwafrika, mtu mweusi, akawafanya wainue mikono

Ikawa hawana budi ila kuitisha majadiliano ya amani

Ela Koitaleli alipoenda kujadiliana na mabeberu akauawa!

Shujaa Koitaleli akauawa kwa mizungu ya Wazungu ya kioga

Unafiki wa wavamizi ukadhihirika wazi na bayana

Hakika mkoloni si mtu mwaminifu

Bali kina Semoi wakachukua nafasi ya shujaa Koitaleli

Mapambano dhidi ya ukoloni yakaendelea

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Tunajivunia Waiyaki

Waiyaki Waiyaki Waiyaki

Waiyaki wa Dagoreti

Chimbuko cha mapambano ya Wakikuyu dhidi ya walowezi

Damu iliyozaa Jeshi la Uhuru na Mashamba, Mau Mau

Kina Waiyaki walipinga unyonyaji wa makampuni ya kibeberu

Walisema hapana kwa ubepari nchini

Hapana kwa mfumo wa kiuchumi wa unyonyaji wa mtu kwa mtu

Walivamia ngome za kupanda mizizi ya mirija ya ubeberu Kenya

Wazalendo wa nchi yetu waliasi kupunjwa na wageni

Walidinda kuwa watumwa wa Wazungu

Wakakataa na utu wa Mwafrika kwa silaha

Waiyaki akakamatwa kuhamishwa Pwani

Wakamshawishi wakamtisha wakamtesa ili asarende

Wapi! wakapiga ukuta kwa babu yetu

Wakashindwa kuumwaga uzalendo wa Mkenya halisi

Wasiweze hata kuukwaruza uhodari wake

Ufashisti wa wakoloni ukazidi kudhihirika Kibwezi

Walipomzika shujaa wetu Waiyaki akiwa hai

Miungu ya nchi yetu

Waingereza walimzika mzalendo akiwa bado anaishi!

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Nyanjiru

Oh Nyanjiru

Tumkumbuke Mary Muthoni Nyanjiru

Yule mwanamke jasiri wa enzi za kiburi cha walowezi

Nyakati za ushujaa wa Harry Thuku

Harakati za wafanyikazi zilipopamba moto

Siku za kukataa kubeba vipande vya wakoloni

Kudinda kulazimishwa kuwafanyia kazi masetla

Kugomea mishahara duni ya kitumwa

Kupinga kunyonywa na kunyanyaswa kwa wanawake

Enzi za chimbuko cha vyama vya kupigania uhuru

Hizo enzi za East African Association

Mapambano ya wafanyikazi katika miji ya nchi yetu

Mapambano dhidi ya kina Colonel Grogan na Lord Delamare

Wakati unyama wa wakoloni dhidi ya wananchi

Ulikuwa ni sehemu ya maisha ya kila siku

Tukitukanwa na kufungwa na kuteswa kiholela

Tukitemewa mate na Wazungu vururumtende

Tukidhihakiwa na kudhalilishwa nyumbani kwetu

Na kina memsahibu walokuwa wakitamba mijini na mashambani

Sisi watu weusi tukifanywa watu wa mwisho

Kana kwamba Kenya si nchi yetu wenyewe

Hizo nyakati za kupinga kulipa kodi kwa wavamizi

Harry Thuku akakamatwa na kuwekwa ndani

Wanaume na wanawake wa Nairobi wakaandamana

Harry Thuku na wafungwa wote wa kisiasa wawachiliwe!

Wafunguliwe mara moja tena bila masharti!

Nje ya Norfolk Hotel

Karibu na Chuo Kikuu cha Nairobi

Si mbali na Central Police Station

Siku hiyo mwaka wa 1922

Kina Nyanjiru walikata shauri kuandamana hapo

Hadi shujaa wao atakapofunguliwa

Hadi Harry Thuku atakapowachiliwa

Wakalala hapo kwa siku na masiku

Baridi ya usiku wakivumilia na njaa na kiu pia

Vitisho vya walowezi wasikubali viwatishe

Bezo za kishenzi za kuuzi za wavamizi wakazipuuza

Na hata wanaume walipozubaa na kusitasita

Walipolegalega na kushindwa kutoa uongozi thabiti

Mary Muthoni Nyanjiru hakulimatia, alijitokeza kimoja

Akadai wanaume wavue surwale na kuvaa skati

Wawape wanawake surwale zao wazivae

Ndipo wanawake wakawa katika msitari wa mbele

Wanaume wakifuata nyuma katika harakati za ukombozi

Pamoja wakasonga mbele kumfungulia mpendwa wao

Pamoja wakaandika historia ya uhuru wetu - kwa damu yao

Shujaa Mary Muthoni Nyanjiru

Akawa wa kwanza kuangushwa na risasi za polisi wa kikoloni

Makaburu waliyokuwa wakistarehe Norfolk Hotel

Huku wakiwatukana na kuwakebehi watu wetu

Wakachukua silaha zao kwa furaha za wehu

Wakaungana na polisi wao kufanya mito ya damu Nairobi

Kutoka kwa mamia ya dada na kaka zetu

Bali yote hayo hayakuuzima moto wa mapambano ya uhuru

Ukaendelea kuwaka moto wa uhuru ukazidi kuzagaa

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Tumkumbuke Makhan Singh

Komredi Makhan Singh, mkomunisti wa kwanza Kenya

Sehemu ya harakati za wafanyikazi dhidi ya ukoloni

Sogora wa mbinu na hila za kuzatiti mapambano

Mapambano ya wavujajasho dhidi ya mabepari

Katika historia ya vyama vya kimaendeleo vya wafanyikazi

Jina la mwanamapinduzi Makhan Singh litang'aa daima

Makhan Singh, sehemu ya kina Chege Kibacia

Chege Kibacia na mashujaa wa watiririkajasho

Makhan Singh,aliyeaminika hata KAU ya Kiburi House

KAU ya Mau Mau katika Kiburi House

Ndiyo, tusisahau Kiburi House

Kiburi House, walikokuwa wakikutana kina Bildad Kaggia

Kina Eliud Mutonyi na kina Isaac Gathanju

Kiburi House, kulikokuwa kukipangwa njama za Mau Mau

Ngome ya waliyochagua barabara ya mapinduzi

Walimtambua Makhan Singh Kiburi House walimhesabu

Kina Makhan Singh na Pio Gama Pinto na Alibhai Mulla Jeevanjee

Wazalendo wa Kenya wa asili ya Kihindi

Waliyowaambia Wahindi wa Kenya

Enyi wananchi wenzetu wa asili ya India

Tahadharini msiwe mapopo na vinyonga

Epukaneni na kuwa makupe na makunguni wa nchi hii

Ikiwa Kenya ni nchi yenu

Kama mnajihesabu raia wa nchi hii

Unganeni na Wafrika kupigania uhuru wa Kenya

Kuweni sehemu ya wazalendo wanaodai ukombozi

Msikubali kutumiwa kunyonya na kufukarisha taifa hili

Kataaeni kuwa upande wa wakoloni na wadhalimu

Msijidanganye kuwa nyinyi ni bora kuliko wenyeji

Wafanyikazi wote tunanyonywa haya shime tuungane

Tuwe na mshikamano dhidi ya wanyonyaji

Tusikubali ubaguzi wa kimbari utuvunjie umoja wetu

Tuugomee ukabila usitumiwe kuondoa uwezo wetu

Wala tusikubali migawanyiko ya kijinsia iturudishe nyuma

Kenya na Uganda na Tanzania wafanyikazi tuwe kitu kimoja

Wafanyikazi wote tupambanie taifa la Afrika Mashariki

Afrika Mashariki ya kimapinduzi

Afrika Mashariki inayopinga ukolonimamboleo

Afrika Mashariki ya mfumo kwa kisoshalisti

Afrika Mashariki itakuwa nguvu kubwa za kisiasa na kiuchumi

Afrika Mashariki itakuwa matumaini ya uhuru na ukombozi kamili

Sauti ya Makhan Singh, sauti ya wanaonyanyaswa

Iliyoitikiwa na wafanyikazi na umma wa wazalendo

Iliwafanya wakoloni kujikojolea na kujiharia

Makhan aliwakosesha mabepari wa Afrika Mashariki usingizi

Jina lake likaandikwa katika kitabu cheusi cha dola la kikoloni

Na hali ya hatari ilipotangazwa rasmi mwaka wa 1952

Makhan Singh hakusahauliwa na kifagio cha polisi wa kikoloni

Makhan Singh alikamatwa mara moja

Makhan Singh akafungiwa kizuizini

Makhan Singh alifungwa miaka kumi kizuizini

Kwa sababu ya harakati za wavujajasho alifungwa Makhan Singh

Alifungwa kwa ajili ya uhuru wa taifa letu

Bali bendera ya wakoloni iliposhushwa Kenya

Na bendera ya Wakenya kupandishwa

Kupandishwa na mapambano ya kina Makhan Singh

Serikali ya msaliti Jomo Kenyatta na mahomugadi

Ilimchukua Makhan kana kwamba si lolote si chochote nchini

Bali kutambuliwa na wanyapara wa mitaji ya mabeberu Kenya

Kupigana pambaja na wanyonyaji na wagandamizaji wa wafanyikazi

Haikuwa nia ya komredi Makhan Singh, mwanamapinduzi

Makhan Singh alikufa akiandika historia ya mapambano

Historia ya mapambano ya wafanyikazi wa Kenya

Makhan Singh ....Makhan Singh....Makhan Singh.......

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Mau Mau

Mau Mau, Jeshi la Uhuru na Mashamba

Kilele cha mapambano dhidi ya ukolonimkongwe

Jazanda ya wazalendo na uzalendo

Mau Mau, mashujaa halisi wa nchi yetu

Wakakataa kutembea katika njia ya kina Jomo Kenyatta

Njia ya wasabili ya kuomba uhuru wa kuomba

Njia ya kutegemea adili ya wagandamizaji

Njia ya kuongozwa na masilahi ya ulafi na uroho

Njia ya kukana mapambano ya silaha katika hali ya ufashisti

Mau Mau wakulima na wafanyikazi wa Kenya

Wanaume kwa wanawake wazee kwa vijana

Walichagua barabara ya kimapinduzi ya uhuru

Mau Mau waliyokula kiapo cha ukombozi

Kiapo cha kuwaunganisha na kuwashikanisha kwa mapambano

Mapambano ya kupigania mashamba na uhuru wetu

Mapambano ya kupigania heshima na utu wa mtu mweusi

Mapambano ya demokrasi na haki za binadamu

Mapambano ya kuung'oa ukoloni nchini kwetu

Maelfu kwa maelfu ya wazalendo wa Kenya

Waliyowacha kila kitu na kuitikia mwito

Mwito wa kujitoma milima Kenya na Nyandarua

Mwito wa kusambaa katika miji na vijiji vya nchi yetu

Kuendeleza vita vya kigorila dhidi ya wakoloni na vibaraka wao

Waliyovumilia njaa na kiu na baridi na upweke na dhiki tilatila

Wakajasiri kuwindwa na kukamatwa na kuhamishwa

Waliyokuwa tayari kuvumilia kukamatwa na kufungwa

Mau Mau, maelfu kwa maelfu waliuawa na wakoloni

Mau Mau, ni wangapi mashujaa wetu waliyonyongwa?

Mau Mau, kiboko cha makaburu na mahomugadi

Mau Mau, kwa damu yenu, kwa kujitolea mhanga kwenu

Enyi wananchi wakereketwa wa taifa letu

Kwa msimamo wenu

Kwa mwelekeo wenu

Kwa harakati zenu

Kwa vita sahihi mlivyopigana

Tuko pahali tulipo sasa, hatua kubwa mbele

Ukolonimkongwe haupo tena nasi, mliukwamua Mau Mau

Kwenu Afrika ikapata mfano mzuri wa kuiga

Mfano wa kupigania ukombozi kwa kutumia silaha

Mau Mau, Jeshi la uhuru na Mashamba

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu ya kila aina

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

Mau Mau

Vilikuwa vita vya kupigania uhuru wa kitaifa

Vita vya wananchi na wananchi kwa ajili ya wananchi

Navyo vita vya wananchi vilizaa mashujaa wengi, wengi sana

Mashujaa waliyochipuka katika msitari wa mbele

Mashujaa waliyoteuliwa na ari na shauku ya kujitolea mhanga

Kujitolea mhanga kutumikia vita vya ukombozi

Mashujaa waliyodhihirisha ujemedari na uhodari

Wa kuongoza jeshi lililokuwa la wananchi wa Kenya

Mashujaa waliyokuwa mashuhuri katika uwanja wa vita

Kwa usanii wa kuzalisha hila na mbinu za kuwachapa maadui

Mashujaa wa siasa na itikadi ya wanaonyanyaswa

Waliyohamasisha umma kwa maneneo na vitendo vyao

Mashujaa wa kutetea haki na ukweli na masilahi ya wengi

Waliyochagua kuishi maisha ya utu ya kupinga dhuluma

Mashujaa kwa mapenzi ya nchi yetu na ukombozi wake

Kwa maendeleo ya Kenya na furaha  ya kila raia

Kwa imani na amani ya wanaonyonywa na kunyanyaswa

Mashujaa waliyokuwa wakipiga konde nyoyo kila wakati

Waliyopambana dhidi ya kulegalega na kukata tamaa

Mashujaa ambao baada ya kukamatwa na wakoloni

Wakiwa mikononi mwa makaburu na mahomugadi

Wakiteswa katika magereza ya wadhalimu wa nchi yetu

Katikati ya ufashisti wa dola la Waingereza

Walivumilia yote kwa ujasiri usiyo na kifani

Walikataa kusaliti kiapo cha kupigania uhuru

Wakadinda kukana vita vya haki vya ukombozi wa Kenya

Wasikubali kutoboa siri wala kusaliti makomredi wao

Na hata waliponyongwa na kuuawa kinyama kabisa

Mashujaa wetu walikufa kwa fahari

Wakawawachia wakoloni na vibaraka wao aibu ya milele

Ni wengi mashujaa wa Mau Mau, wengi sana

Kwani Mau Mau ni wanati, wananchi wazalendo wakereketwa

Mau Mau, ushujaa wa mamilioni

Ya wakulima na wafanyikazi

Wanaume kwa wanawake wazee kwa vijana

Ambao kwa moyo wa harambee uzalendo na kujitegemea

Walifunga sura  ya ukolonimkongwe katika nchi yetu

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu ya kila aina

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Kimaathi

Dedan Kimaathi

Dedan Kimaathi wa Waciuri

Mkuu wa jeshi la Uhuru na Mashamba

Kati ya majemedari wa Mau Mau Kimaathi ali ni gogo

Baina ya mashujaa wa uhuru hakika Dedan Kimaathi ni nyota

Nyota iliyoonekana na inayoonekana katika kila pembe ya Kenya

Nyota inayong'aang'aa Afrika kuonyesha barabara sahihi

Barabara ya kimapinduzi ya kuelekea kwa uhuru

Nyota mashuhuri Afrika na hata duniani kote

Kwa wanaonyonywa na kugandamizwa

Oh pande la mwana wa Kenya, ndugu yetu mpendwa Kimaathi

Ni maneno gani tutayatumia  ewe mwana wa Waciuri

Hata tukaeleza  sifa zako tilatila kwa kikamilifu?

Ninashindwa hata kupata nahau bora

Za kuandika kuhusu Mkuu wa Jeshi la Uhuru na Mashamba

Pengine niseme tu kuwa Kimaathi alikuwa mtu

Alikuwa mtu Kimaathi, mtu kama sisi

Alikuwa na mamaye na babaye na bibiye na babuye

Alikuwa na jamaaze, damuze, kama sisi

Alikuwa na mke, mke aliyempenda sana, tena sana

Kimaathi alikuwa kijana, kijana  kama sisi

Kijana aliyetambua jukumu lake kama mwananchi mzalendo

Mtu ambaye alifahamu yu mtu kwa maneno na matendo

Kimaathi, maana ya mapenzi kwa nchi yako na watu wake

Kimaathi, mfano halisi wa ushujaa wa kimapinduzi

Ushujaa wa umma uhodari wa masilahi ya wanaogandamizwa

Kimaathi, twasira na jazanda ya kujitolea mhanga

Kwa uhuru na ukombozi wa kitaifa

Kati ya wasanii wa hila na mbinu ya vita vya kigorila

Kimaathi wa Waciuri anatajika kama sogora mkubwa

Kati ya majina yaliyokuwa yakiogopewa na wakoloni

Jina la Dedan Kimaathi lilikuwa namba wani

Kimaathi aliwafanya makaburu kujikojolea na kujiharia

Wanyonyaji wakashindwa kula manyonyaji yao kwa amani

Wangapi walowezi walifungasha na kuondoka

Kwa kuogopa Kimaathi, asakari hodari wa Mau Mau!

.....ahhhh! lakini nani asiyemfahamu Kimaathi nchini!

Ni mwananchi gani mzalendo ambaye hajui Mau Mau!

Ni historia gani ya Kenya hiyo ambayo haitaji Mau Mau!

Ni mashujaa gani wa Kenya unawajua kama humjui Kimaathi!

Hakika katika kuandika historia sahihi ya taifa letu

Hatutawasamehe kina Ndirangu Mau milele

Kina Ndirangu Mau - mahomugadi waliyomsaliti shujaa wetu

Kina Ndirangu Mau - kina Kenyatta na Moi wenye dola la kisaliti

Kina Ndirangu Mau - wanyonyaji wa wakulima na wafanyikazi

Kina Ndirangu Mau - vibaraka wa mabeberu

Kina Ndirangu Mau - wanaopinga ukombozi wa taifa letu

Tutawasemehe vipi kwa kuendelea kukataa kumzika Kimaathi!?

Mnamo tarehe 18  Februari mwaka wa 1957

Katika Jela ya Nairobi

Dedan Kimathi wa Waciuri, shujaa mkuu wa Kenya

Alinyongwa na wakoloni wa Wingereza

Alinyongwa baada ya mateso ya kifashisti ya kina Ian Henderson

Alinyongwa huku akipambana akiwa na pingu mikononi

Shujaa wa nchi yetu alikufa akipigana

Mwili wa Kimaathi ulitupwa na wakoloni

Katika Jela ya Kamiti

Na hadi wa leo

Mazishi ya Mzalendo Kimathi

Yanangojea kufanywa, tukumbuke

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu ya kila aina

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Mathenge

Stanley Mathenge

Jemedari Stanley Mathenge

Sehemu ya shina na mzizi wa Mau Mau

Komredi mkuu wa Kimathi

Mzalendo Stanley Mathenge

Naye daima hatutamsahau hakika

Kwani yu shujaa wa uhuru wa nchi yetu

Msituni alitambulikana kwa uadilifu na ukakamavu

Daima alikuwa tayari kufa akitetea haki na ukweli

Kwa wakoloni na mahomugadi na wasaliti wote

Mathenge alikuwa hatari kwa usalama

Kwa maaskari wa Mau Mau

Mathenge ali kamanda wa kutegemea

Kwa wananchi wa Kenya

Kina Mathenge ni jazanda la matumaini

Mathenge alikuwa tayari kufa kuliko kusarenda kwa ukoloni

Mashambulizi ya jeshi la kikoloni yalipokuwa mno

Mabomu ya ndege za wakoloni yalipozidi usiku na mchana

Hata yakatisha kugeuza milima Kenya na Nyandarua jangwa

Tatizo la Mau Mau la kukosa silaha za kutosha lilipokuwa mno

Wasaliti walipopenya hadi ndani ya misitu katikati ya Mau Mau

Yasemekana kina Mathenge waliamua kutoka msituni

Kutoka msituni na kukimbilia Kaskazini mwa nchi yetu

Wengine walisema kuwa kina Mathenge walifika Ethiopia

Hatuna hakika, serikali ya mahomugadi ya Kenyatta na Moi

Haina haja ya kujua ukweli - ukweli kuhusu kina Mathenge

Ela ukweli ni kwamba

Mathenge alikataa katakata kuwainulia wakoloni mikono

Alikuwa tayari kufa kuliko kusarenda Mathenge

Popote alipoenda

Alienda akiwa mzalendo wa Kenya

Hakuwacha kuwa shujaa wa umma Mathenge

Kina Mathenge na Mau Mau

Pandikizi za watu

Wazalendo tuna kazi kubwa

Kazi ya kumtafuta Mathenge, kina Mathenge

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu ya kila aina

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

Kago

Kariuki Kago

Jemedari Kariuki  Kago

Mwana wa maskwata

Maskwata waliyoporwa mashamba yao na walowezi

Mamilioni ya wakulima makabwela wa Kenya

Waliyotimuliwa na masetla wa kikoloni

Kutoka kwa ardhi yao ya jadi

Wakigeuzwa mafukara na walalahoi

Wananchi wasiyo na hata inchi ya nchi yao

Shujaa Kariuki, Kago Kariuki alichukia ukoloni mno

Ali akichemka kwa hasira ghamu na ghamidha

Ali akisisimuka na kutetemeka kwa ghadhabu

Alifahamu uchungu na aibu ya kutawalwa na Wazungu

Akakataa kuketi na kulia na kulalamika bila vitendo

Ndipo kibirikizi cha Mau Mau kilipolia Kago alikisikiliza

Alikisikiliza akajitoma katika msitu wa Nyandarua na silaha

Kuungana na wanaume na wanawake wa vitendo halisi vya uhuru

Katika uwanja wa vita vya kigorila Kago ana sehemu

Alionekana bayana kwa ujasiri na uhodari wake

Alikuwa sogora wa mbinu ya kuvizia na kushambulia ghafla bin vuu

Kina Kago kwa uhodari na ujemedari wao

Waliwaweza wakoloni na dola lao

Mnamo mwaka wa 1954 mwezi wa Machi

Kago, ndugu yetu mpendwa Kago, aliuawa na maadui

Katika msitari wa mbele

Alikufa kifo cha shujaa na bunduki ya haki mikononi

Wakati minara ya mashujaa itakapojengwa

Mwingine utakuwa wa Kago

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu ya kila aina

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Kariba

Kariba (Hituchi Kabutu)

Jemedari Kariba wa kikosi cha Hika Hika

Simba wa Mathira na Tetu

Kariba alikuwa kiboko cha makaburu na mahomugadi wa Nyeri

Aliwasisimua na kuwahamasisha wengi kusimama imara

Katika msitu wa Kirinyaga

Jemedari China

Katika enzi za ushujaa wake

Alimwamini Kariba kama mchapaji kazi ya vita vya ukombozi

Kariba, mfano wa vijana tunaowahitaji leo

Mnamo Oktoba mwaka wa 1954 alikamatwa na polisi wa kikoloni

Kariba akashawishiwa akatishwa akateswa kuteswa

Bali shujaa wa vita vya umma akakataa kukana Mau Mau

Akadinda kabisa kuwalilia na kuwaomba maadui

Kariba asikubali kusaliti vita vya haki vya ukombozi

Siku utenzi wa mashujaa wa uhuru wa Kenya utakaposomwa

Beti kadhaa zitakuwa za Kariba

Mnamo Alhamisi tarehe 6 Januari mwaka wa 1955

Jemedari Kariba

Mkuu wa kikosi cha Hika Hika

Akanyongwa na wakoloni

Mzalendo Kariba

Alichinjwa na wakoloni katika Jela ya Nairobi

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu ya kila aina

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Tanganyika

Muriuki Kimotho - Jemedari Tanganyika

Tanganyika naye ni twasira ya ushujaa na uhodari

Na tena  yu kamusi ya maana ya uzalendo na kujitolea mhanga

Akiwa amebaki kiongozi wa kikosi cha Hika Hika

Huko Mlima Kenya

Tanganyika alidhihirisha uongozi thabiti wa ukakamavu

Mashambulizi ya wakoloni na mahomugadi yaliyochacha

Mabomu kutoka kwa ndege za ufashisti wa Wingereza yaliyozidi

Dhiki za maradhi na njaa na baridi zilizoongezeka mno

Ukosefu wa silaha uliyokuwa tabu kubwa kwa Mau Mau

Usaliti wa Jemedari China uliyokuwa pigo kubwa kwa Mau Mau

Haya yote Tanganyika alipambana nayo bila kukata tamaa

Tanganyika alikataa katakata

Kuwacha harakati za ukombozi bila ukombozi

Aligoma kuutambua utawala wa wakoloni katika nchi yetu

Hakukubali kushirikiana na vibaraka wa wakoloni

Alikamatwa mnamo tarehe 10 mwezi wa Aprili mwaka wa 1956

Muruiki Kimotho alikamatwa na kutiwa ndani na wakoloni

Akashawishiwa akatishwa akafanyiwa unyama usiyo na kifani

Bali ndugu yetu akakataa kuwalilia na kuwaomba wakoloni

Tanganyika asikubali  hata kidogo

Kujuta kwa kutekeleza jukumu lake la kizalendo

Akashikilia vita vya ukombozi ni vita halali

Mapambano dhidi ya dhuluma ni ya ukweli na haki

Wakati tutakapotunga nyimbo za kuimba sifa za mashujaa wetu

Jina la Tanganyika litasikika kwa fahari katika maghani yetu

Mnamo tarehe 6 mwezi wa Julai mwaka wa 1956

Tanganyika akanyongwa katika Jela ya Nairobi

Muriuki Kimotho akaungana na maelfu ya mashujaa wetu

Waliyotoa maisha yao kuwa matambiko

Ya uhuru na ukombozi wa taifa letu

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu ya kila aina

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Mukami

Alice Mukami

Alice Mukami Kimaathi

Mzalendo Alice Kimaathi

Askari hodari wa Mau Mau

Mukami gorila mashuhuri mijini na vijijini na msituni

Mukami kiongozi wa kikosi kabambe cha wanawake

Mukami na wanawake, wanawake wazalendo wa Mau Mau

Mbiu ya mgambo ilipolia kutangaza vita vya uhuru na mashamba

Vita vya kupambana dhidi ya wakoloni na mahomugadi wao

Mukami hakusitasita aliamua kimoja

Akafuatana na mumewe Kimaathi kwa hiari yake mwenyewe

Akawa sehemu ya maelfu ya wanajeshi wanawake wa Mau Mau

Waliyokuwa sababu ya ufanisi mkuu wa Mau Mau

Mukami alitambua jukumu lake

Kama Mkenya na kama binadamu

Kweli Mukami ni jazanda la ushujaa wa wananchi

Siku ya kuwapamba mashujaa wa uhuru wa Kenya itakapofika

Tutampamba Mukami kwa dhahabu na almasi

Anaishi hadi wa leo Mukami anaishi kwa uzalendo

Serikali ya mahomugadi wa jana na leo inayotutawala

Inaendelea kumnyanyasa mama yetu mpendwa

Inakataa kumuonyesha Mukami kaburi la mumewe Kimaathi

Maadui wakubwa wa uhuru na ukombozi wa taifa letu

Wanaovuruga na kuparaganya historia yetu ya mapambano

Wanaendelea kukana Mau Mau na kina Alice Mukami

Wanaendelea kuwashindilia katika kasumba ya dini

Bali kina Mukami

Hawana haja ya kutambuliwa na wasaliti wa Mau Mau

Wanafahamu

Ingawa juhudi zao ziliung'oa ukolonimkongwe

Mapambano bado yanaendelea

Kwani ukolonimamboleo ungaliko

Mukami, bado kina Mukami wanahitajika

Na watahitajika milele

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

J.M.

Josiah Mwangi Kariuki

Mzalendo Josiah Mwangi Kariuki

Mau mau kizuizini

Sauti ya Mau Mau bungeni

Jina linaloendelea kuufafanua u-Mau Mau

U-Mau Mau katika enzi za ukolonimamboleo

Josiah Mwangi Kariuki, Mau Mau kizuizini

Wakati kibirikizi cha Jeshi la Uhuru na Mashamba kilipolia

Kilipolia kuwaita wazalendo wajitokeze wawajibike

Wawajibike kwa ajili ya uhuru na ukombozi wa Kenya

J.M. hakusitasita wala hakulegalega

Alijitokeza kimoja kutekeleza jukumu lake

Jukumu lake kama mwananchi na mzalendo mkereketwa

J.M. akawa sehemu ya Mau Mau

Alipotiwa mbaroni na kufungwa kizuizini

Pamoja na mateso yote aliyoteswa

Pamoja na vitisho vyote alivyotishwa

Pamoja na vishawishi vyote alivyoshawishiwa

Pamoja na unyama wote waliyofanyiwa wafungwa wa kisiasa

Pamoja na magumu yote waliyoyakula Mau Mau kizuizini

JM alikataa kabisa kukana mapambano ya uhuru

J.M. alidinda wakati wote kusaliti Mau Mau

Asikubali hata kidogo kujuta kwa msimamo aliyouchukua

Gerezani akawa taswira ya matumaini na kupiga konde moyo

Na akatoka kizuizini akiwa mzima kama kigongo

Tayari kuendelea na mapambano ya uhuru kamili

Mwaminifu kwa maadili ya Jeshi la Uhuru na Mashamba

J.M. akawa sauti madhubuti ya kusema

Hatukupigania uhuru ili tuingie nafasi ya wakoloni

Hatukupambana ili kunyang'anyana mashamba na maploti

Hatukuingia msituni ili kuteseka na kufa

Kwa ajili ya mahomugadi wa jana na leo

Wala hatukufungwa na kula ngumu

Ili kuleta mfumo wa unyonyaji wa mtu kwa mtu

Hatuwezi kujivunia Kenya ya mamilionea kumi

Na maskini milioni kumi

Tulikataa unyonge wa kunyanyaswa na kina Lodi Delamare

Na huu wa kugandamizwa na kina Jomo Kenyatta hatuutaki pia

Josiah Mwangi Kariuki

Pamoja na utajiri wake wote

Akajipiga kitanzi cha kitabaka

Na kuwa upande wa wengi wanaonyonywa

Bungeni akawa mwakilishi halisi wa mamilioni ya Wakenya

Kwa msimamo wake akawa sumu

Kwa utawala wa kisaliti wa Kenyatta

Mkenya kwa kila hali

Daima aliulani ukabila na ubaguzi wa rangi

Komredi wa wafanyikazi siku zote

Aliupinga mfumo wa ubepari

Mwandishi wa uzalendo wa Mau Mau

Josiah Mwangi Kariuki alipendelea uchumi wa kisoshalisti

Alipambania uchumi wa kitaifa

Wa haki na unaojitegemea na kujiendeleza

Ndiyo kwa maana serikali ya kigaidi ya Kenyatta na kanu

Mnamo mwaka wa 1975

Ilimuua J.M.

Kinyama kabisa

Na kutupa mwili wake

Katika msitu wa Ngong’ ili uliwe na fisi

Lakini hata fisi wenyewe

Walimheshimu J.M. kwa ushujaa wake

Fisi wakakataa kabisa kumla ndugu yetu mpendwa!

Maiti ya Kariuki yakapatikana

Uhalifu wa Kenyatta ukabainika hata zaidi

Serikali ya wasaliti ikatingishika

Wingu la huzuni likafunika nchi yetu

Mvua ya machozi ya majonzi ya wazalendo

Ikanyesha Kenya nzima na hata Afrika Mashariki

Kilio cha Wakenya kikasikika duniani kote

Mzalendo Josiah Mwangi Kariuki

Tukamfanyia mazishi ya shujaa wa umma

Tukamzika komredi wetu kwa vifijo na ndremonderemo

Na tukaamua kutowasamehe wauwaji wake milele

Na tarehe 3 Machi

Tukasema ni siku ya J.M.

Josiah Mwangi Kariuki

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Tusisahau enzi za makumi ya themanini

Nyakati za ukolonimamboleo

Mfumo wa usaliti wa Moi na kanu

Udikteta ulipotia fora katika nchi yetu

Tukawa ja tu chini ya ufashisti

Mipango halisi ya dola la imla

 Kuhofisha na kushurutisha

Na kuamrisha na kugandaniza na kunyanyasa

Udhalimu ukahalalishwa na kurasimishwa kikatiba

Mfumo wa chama kimoja cha KANU cha kanu

Sheria za uchochezi na uhaini

Zikafunguliwa dhidi ya raia

Haki ikikanyagwa na kuvunjwa kiholela

Ukweli ukipakwa matope na kudharauliwa

Utu wa mtu ukipuuzwa na kufanywa si kitu

Wenye nguvu za dola wakigeuka wanyama

Hayawani dhidi ya binadamu na ubinadamu

Mahakama yakigeuzwa kuwa ya bandia

Kenya ikawa chini ya mfumo wa imla kisheria

Chama cha kanu cha kutawala kwa tuteni

Chama cha kupinga uhuru na maendeleo

Chama cha wanyonyaji wezi na wafisadi

Chama cha vibaraka na vibarakala

Chama cha genge la wajinga na wakora

Chama cha waporaji wa mali ya umma

Chama cha Kanu

Kanu ya Moi

Moi wa kufuata nyayo za Jomo Kenyatta

Kenyatta aliyesaliti uhuru wa taifa letu

Kwa ulafi wa pesa na unyakuzi wa mashamba

Kwa uroho wa mali za duniani

KANU ya kanu

 Mtu mmoja akitawala Kenya

Kana kwamba ni shamba lake binafsi

Akinyakua kila alichokitamani

Pamoja na wanawe na vibaraka wake

Ikawa lazima kila raia awe chini ya chama cha Kanu

Vyombo vya dola vikitumika

Kuulinda na kuuimarisha utawala wa mabavu

Polisi na mahakimu na magereza na utawala wa mikoa

Wakitekeleza amri za kishenzi na kikatili

Amri za kupambana dhidi ya uhuru wa wananchi

Amri za kupinga na kukataza haki za binadamu

Amri za kutekeleza sheria za katiba ya udhalimu ya kikoloni:

Kusiwe na chama kingine isipokuwa cha kanu

Kusiwe na siasa zozote isipokuwa za kanu

Kusiwe na viongozi wowote isipokuwa wa kanu

Kusiwe na mikutano yoyote bila ruhusa ya machifu wa kanu

Kusiwe na uchaguzi wowote isipokuwa wa viongozi wa kanu

Rais Moi akiwa jitu shetani bin ibilisi

Kusiwe na rais yoyote isipokuwa Moi

Kusiwe na habari zozote bila kutaja Moi

Kusisifiwe mtu yoyote mwingine ila Moi

Kila kitu kiitwe Moi au Kenyatta

Kwaya na ngoma zote ziimbe na kumsifu Moi

Maombi yote yaombewe Moi

Kusiwe na maswali yoyote ila kutii amri

Amri kutoka kwa Moi

Ikawa kukosoa rais au serikali

Ni uchochezi ni uhaini

Kuukemea ufisadi na ubepari na ubeberu

Ni kosa kubwa kuliko unyang’anyi

Tukawa kama watumwa

Katika nchi yetu wenyewe

Usiku na mchana

Tukisakwa na kuwindwa

Tukiishi kwa hofu na wasiwasi

Tukikamatwa kuteswa kushtakiwa na kufungwa kiholela

Wasomi wazalendo wakifutwa kazi na kuwekwa vizuizini

Viongozi wa wanafunzi wazalendo wakifukuzwa vyuoni

Migomo ya wafanyikazi

Ikivunjwa kwa mitutu ya bunduki

Usanii wa kizalendo ukipigwa vita mbele na nyuma

Majasusi wakiwekwa kila pahali

Mijini na mashambani

Afisini na viwandani na mitaani

Kazi kubwa ya polisi

Ikawa ni kupambana dhidi ya waasi

Waasi wa uongozi wa giza na kifo

Waasi wa utawala wa Moi na kanu

Waasi wa mfumo wa ubepari na ukoloni mamboleo

Waasi wa utamaduni wa hofu na kimya

Waasi wa maadili ya kuabudu pesa na mali

Waasi wa nyanyaso na gandamizo

Waasi wa ufisadi na usaliti wa taifa

Waasi wenye kudai mageuzi

Mageuzi ya kuondoa mfumo wa ubepari

Mageuzi ya kuleta uhuru na demokrasi

Mageuzi ya kujenga mfumo wa usoshalisti

Magereza yakajaa wazalendo na wanamapinduzi

Wengi wakisukumwa uhamishoni

Kwa kuzidi kwa nyanyaso

Uchumi ukazidi kuporomoka

Kwa kuparaganywa, kuhujumiwa na kuporwa kiholela

Uporaji wa mashamba na maploti na mashirika ya umma

Ukawa sehemu ya maisha ya kila siku

Barabara zikinyakuliwa

Misitu ikinyakuliwa

Pwani zikinyakuliwa

Mito ikinyakuliwa

Vinamasi vikinyakuliwa

Maziwa yakinyakuliwa

Visiwa vikinyakuliwa

Viwanja vya michezo vikinyakuliwa

Shule zikinyakuliwa

Makaburi yakinyakuliwa

Hata vyoo vya umma vikinyakuliwa

Kisibaki kisichokuwa na hatari ya kunyakuliwa

Unyakuzi unyakuzi unyakuzi unyakuzi

Ukifukarisha wakulima makabwela mashambani

Na kuzidisha mitaa ya mabanda mijini

Ukosefu wa kazi ukizidi na kuzidi na kuzidi

Bali

Upinzani kwa upande wake

Ukakua na kukua na kukua na kukua

Wala usisite kukua

Kila siku ukakua

Ukakua vyuoni na viwandani pia

Mijini ukakua na mashambani vilevile

Wazalendo wakikutana

Hadharani na mafichoni

Wakijipanga na kujizatiti

Mara juu kwa juu na mara chini kwa chini

Wakajitolea mhanga

Kupigania ukombozi

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Ndiyo, tusiwasahau wazalendo

Waliyojitolea mhanga kufa na kupona

Kwa udi na uvumba

Kupambana dhidi ya udikteta wa Moi na Kanu

Na kudai uhuru na demokrasi na Katiba ya Kenya

Wakipambania mfumo wa ujamaa

Hawa ni mashujaa wa kweli wa uhuru

Wanastahili kuandikwa kwa historia

Tuwaonee fahari milele na milele

Kwa kuvumilia mengi magumu na mazito na machungu

Kwa ujasiri na ukakamavu

Kwa kupambana pasina kukata tamaa

Wakishikilia nyoyo za matumaini

Huku wakikumbuka Mau Mau

Wakaleta ushindi dhidi ya imla hatimaye

Utawala wa mfumo wa chama kimoja cha kanu

Ukaanguka ukachunuka ukaondoka ukahiliki

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu tilatila

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

December Twelve Movement - DTM

Mwakenya

Wali ni wazalendo na wanamapinduzi

 Vijana na wazee

Wanafunzi wa vyuo vikuu

Walimu wa taasisi mbalimbali

Wafanyikazi na wakulima

Kutoka sehemu mbalimbali za Kenya

Ambao waliamua kuunda chama

Chama cha chini kwa chini

Wakiandika kuchapisha na kusambaza Pambana

Pambana kutoka Wangige Kibichiku na Momoto

Pambana gazeti la DTM

Pambana sauti ya mapambano

Mapambano dhidi ya utawala wa imla

Mapambano dhidi ya ufisadi na uporaji wa mali ya umma

Mapambano dhidi ya ubepari na ubeberu

Mapambano ya kupigania mfumo wa kisoshalisti

Pambana jarida la uchochezi

Kuwachochea umma unaonyonywa na kunyanyswa

Uamke uungane ushikane utende

Wakenya wasikubali kugawanywa kikabila

Pamoja wapambanie ukombozi wao

Watambue msingi wao wa kitabaka

Waishikilie itikadi ya ukombozi kamili

Itikadi ya kisoshalisti

Kuwachochea wanafunzi na wasomi

Wagomee utawala wa kijinga na kimabavu

Kuwachochea wafanyikazi

Wajizatiti wapiganie masilahi yao na ya jamii

Kuwachochea wakulima makabwela na maskwata

Wadai mashamba na maploti

Kuwachochea wadhulumiwa wote

Wachukie dhuluma na wadhalimu

Na Mpatanishi

Kuli na Mpatanishi pia

Gazeti la wanachama wa DTM

Mpatanishi gundi la wanachama

Mpatanishi kuwapatanisha wanamapinduzi

Kutoka kila sehemu za nchi yetu

Mpatanishi kuleta umoja wa wanamapinduzi

Mpatanishi kujadili nadharia na itikadi

Mpatanishi kusambaza elimu ya kikomunisti

Mpatanishi kuzatiti na kupanga mbinu na hila

Mpatanishi siri ya DTM

Wanachama wakichangia Pambana na Mpatanishi

Kila mwanachama akitoa kwa harakati

Asilimia fulani ya mapato yake

Si wafanyikazi si wakulima si wanafunzi

Kila mtu alitoa kile alichokiweza

Kuyadhamini mapinduzi

Kili ni chama cha wanachama kwa hali na mali

Watu wazuri sana tena waadilifu

Waliyouchukia ukabila na ubaguzi wa aina yoyote ile

Waliyotambua jukumu lao la kihistoria

Na kutenda ipasavyo

Waliyotambua ukweli halisi

Mfumo wa udhalimu hautaondoka wenyewe

Ni mpaka uondolewe

Uondolewe kwa mipango na mapambano

Mapambano ya wazalendo na wanamapinduzi

Yaliyoukosesha usingizi

Utawala wa Moi

Ndipo naisifu DTM pamoja na Mwakenya

Nasema historia yake

Nikiimba sifa za mashujaa wake

Maana ni jukumu langu

Kwani historia sahihi ya mapambano ya uhuru

Haitaandikwa na wasaliti wa jana na leo

Mashujaa wa kweli wa nchi yetu

Hawatatambuliwa na serikali ya wasaliti

Na hakika mashujaa wa umma

Wanastahili kukumbukwa

Tuwaonee fahari na kuwasifu

Kwani ni mfano mwema wa kuiga

Tena ni ngome ya mtima wa matumaini

Na tochi ya kuangazia leo

Na pia kumulika siku zijazo

Ndiyo

Tuwakumbuke

Mashujaa wa nchi yetu

Wazalendo halisi wa Kenya

Jinsi walivyokuwa wamejitolea mhanga

Kupambania uhuru na ukombozi wa nchi yetu:

Na sisi leo

Lazima tupambane kwa vyovyote vile

Tujikaze kisabuni

Mateso na majaribu ya kila aina

Tunayaona

Na tutaendelea kuyaona

 

Mwandawiro Mghanga

Jela Kuu ya Kibos    Aprili 6 1988

 

 

                Mnafiki

                                   uwongo wako!

hata kama ni kweli

ulipigania uhuru

hata kama ni hakika

ulikuwa kwa Jeshi la Uhuru na Mashamba

hata kama ulisema nini na kufanya kitu gani

dhidi ya ukolonimkongwe

ikiwa sasa wewe ni msaliti

ikiwa wakati huu u kibaraka cha mabeberu

ikiwa leo wewe ni mnyonyaji

kama u mbakuzi wa mashamba na maploti

endapo unaunga mkono mfumo wa unyonyaji wa mtu kwa mtu

ikiwa unadai kuna uhuru Kenya leo

hakika kabisa wewe si shujaa wa wananchi

wala usifikiri u mzalendo hata kidogo

 

kwani ulafi wako

tamaa ya mali na pesa

ubinafsi

unafiki na ubarakala wako

umefuta historia yako safi ya jana

kweli huwezi kutudanganya tukadanganyika

wala huwezi kusema tukakusikiliza

katika historia ya leo ya nchi yetu

wewe si rafiki wa mapambano ya ukombozi wa kijamii

leo umegeuka kuwa adui, unapinga maendeleo ya nchi yetu

kwa kuwa umekubali kuwa mbwa wa wakolonimamboleo

kwa sababu unazungumza lugha ya wagandamizaji

 madhali unatetea mfumo wa ubepari

maana leo u fisi na nguruwe

maadamu sasa u sawa na kupe na kunguni

kwa vile u malaya mkubwa siku hizi

 

shujaa wa kweli wa umma

mzalendo halisi

husafiri hadi mwisho wa safari

na safari yetu ya mapambano bado ingaliko

haijafika mwisho wake safari yetu ya uhuru na maendeleo

kwani ukolonimamboleo ungaliko katika nchi yetu

wananchi tunaumizwa na udikteta wa kanu

ingawa bendera inapepea uhuru wenyewe bado

kumbe wewe ulikuwa ukipambania tumbo lako tu

kumbe nia yako ilikuwa kuchukua nafasi ya mkoloni

tulikataa unyonge wa kunyanyaswa na Waingereza

unafikiri tutaikumbatia aibu

ya kudhulumiwa na Wafrika wenzetu?

shetani mkubwa wewe!

msaliti unayechafua jina safi la Mau Mau!

mzandiki!

 

Mwandawiro Mghanga

                                        Jela Kuu ya Kibos  Oktoba 25 25 1988

  The Rural Woman: Not to Be Celebrated—But Liberated
24 Nov 2025 06:00

                                                                  peech on the Peasant Women Day, 15th October, 2025. Written by Leon Munala Secretary of The Peasants and Peasant Organization Delivered by Comrade Karimi Wa Kagendo National Organising Secretary, Revolutionary Youth League Comrades, sisters, and fellow workers! Today, the representatives of global capital in their glass palace tells us to celebrate. The United Nations, that grand committee for managing the common affairs of the global bourgeoisie, has  [ ... ]

Read more
FROM THE COMMUNE TO THE PEOPLE’S POWER: ANTI-IMPERIALIST STRUGGLE AND THE PATH O...
12 Nov 2025 08:41

    Booker Omole General Secretary, Communist Party Marxist Kenya (CPMK) October 17th, 2025 Caracas, Venezuela   omuna o Nada: The Question of Power in the Age of Imperialist War Comrades, the slogan “Comuna o Nada” — the commune or nothing — is not merely a Venezuelan proclamation; it is a universal cry of the proletariat in our epoch of crisis. It affirms that without transforming the relations of production, without uprooting imperialist domination, and without transferring power from the exploiting classes to the working people, there can be no socialism.   Today, [ ... ]

Read more
OFFICIAL STATEMENT ON THE FASCIST OFFENSIVE OF IMPERIALISM IN TANZANIA UNDER PR...
05 Nov 2025 14:01

November 2, 2025   The Communist Party Marxist Kenya stands with the people of Tanzania in this moment of heightened danger. The ruling class across East Africa is tightening the chains of monopoly finance capital. The mask of liberal democracy is falling. Behind it stands naked reaction. Behind it stands fascism in African colours.   President Samia Suluhu Hassan has presided over political developments marked by aggressive interference from foreign capital. We are witnessing new assaults by the corporations and financial institutions headquartered in the old imperial centres. They want [ ... ]

Read more
STATEMENT ON THE PASSING OF COMRADE KIM YONG NAM COMMUNIST PARTY MARXIST KENY...
05 Nov 2025 13:51

    November 5, 2025   The Communist Party Marxist Kenya conveys its deepest condolences to the Workers Party of Korea, the Government of the Democratic People’s Republic of Korea, and the heroic Korean people on the passing of Comrade Kim Yong Nam, former Chairman of the Standing Committee of the Supreme People’s Assembly.   Comrade Kim Yong Nam was not merely a statesman. He was a defender of sovereignty. He was a guardian of independence. He was a steadfast revolutionary in the global front against imperialism.   Throughout his service to the Party and the State, the Dem [ ... ]

Read more